Friday, June 19, 2015

Usikubali kuwa chanzo cha mpenzi wako kukusaliti


Rafiki, wanawake wengi hulia na kujutia kuwepo katika ndoa, hii ni kutokana na kuhisi au kujua kuwepo kwa usaliti kwa waume zao. Ukweli ni kwamba suala la kusalitiwa linaumiza sana, hakuna atakayekuwa tayari kukubali usaliti katika penzi lake.
Huo ndiyo ukweli, lakini pamoja na ukweli huo umewahi kujiuliza kwa nini mpenzi wako anakusaliti? Umewahi kufikiri kwamba hata wewe unaweza kuwa chanzo cha mpenzi wako kukusaliti?



Kama hujawahi kufikiri basi fahamu kwamba kama usipokuwa makini katika maeneo fulani katika ndoa yako, unaweza kuwa chanzo cha mumeo kukusaliti. Vipengele vifuatavyo, vinafafanua hilo kwa undani zaidi: 

UNATAMBUA MAJUKUMU YAKO?
Hili linawashinda wengi katika maisha ya ndoa na waume zao kwa kukosa kujitambua kuwa yeye ni nani na wajibu wake katika ndoa yake ni upi. Hapo awali kabla ya kuingia katika ndoa na mumeo ulikuwa ukimnyenyekea na kujitahidi kadiri ya uwezo wako kumwonyesha mapenzi motomoto lakini sasa baada ya kuingia katika ndoa umebadilika.

Ulikuwa msafi mwenye kumjali wakati wote na kumwonyesha kuwa yeye ni muhimu maishani mwako na wewe ni muhimu sana katika maisha yake. Kuwa naye karibu wakati wote na kumshauri hasa akiwa katika matatizo na sononeko la moyo au msongo wa mawazo vilimvutia na kuona thamani yako kwenye maisha yake.

Huenda hapo awali ulikuwa mshauri wake mkubwa wa mambo mbalimbali ya kikazi na wakati mwingine mambo yake binafsi, wakati alipokuwa na majaribu ya kufukuzwa kazi au kupata balaa la madeni kazini kutokana na uharibifu au upotevu wa mali ya anapofanyia kazi kwa kumshauri au hata kumsaidia kifedha.

Sababu hizo na zingine nyingi ulizokuwa ukimfanyia wakati mkiwa wachumba huenda ndizo zilizomsukuma akusogeze karibu ili aishi na wewe kwa kutambua umuhimu wako katika maisha yake lakini sasa umebadilika!

Mwanaume anahitaji mwanamke wa kumshauri na kumpa moyo hasa anapokuwa kwenye majaribu na matatizo mbalimbali ya kimaisha.

Kama awali ulikuwa ukimfanyia hivyo mumeo na sasa umeacha ni wazi kwamba atakapokuwa na msongo wa mawazo au matatizo flani atakwenda baa ambako atakutana na mwanamke wa nje na akithubutu kumweleza yaliyomsibu atapata tulizo kwa sababu wanawake wa nje ni mahodari wa kufariji waume za watu.

Baadhi ya wanawake wakishaingia katika ndoa, hujisahau na kuona kuwa wao ni wao na kama walichotaka wameshakipata hivyo kujisahau na kutowapa wapenzi wao mapenzi motomoto. Kikubwa unachopaswa kutambua wewe mwanamke ni kwamba wanaume wanapenda kuona wake zao wanakuwa kwa ajili yao na kuwafanyia vituko vya mahaba kila wakati.

Kadhalika hupenda kuona wake zao wanakuwa karibu nao wanapokabiliwa na matatizo mbalimbali ya kimaisha. Hakika utakaposhidwa kumjali mumeo huona ni afadhali atafute kitulizo kingine ambapo hata hivyo mara nyingi hukimbilia baa kutafuta kitulizo cha msongo wa mawazo.

Wengine hushinda kutwa nzima nyumbani wakihudumia mifugo au wakifanya shughuli ndogondogo za kila siku kama kufua, kupiga deki na kazi nyingine za mama wa nyumbani baada ya hapo hubaki na nguo alizoshinda nazo kutwa nzima hadi mumewe anaporejea kazini humkuta akiwa na nguo hizo chafu huku akinuka jasho ambapo kwa kiasi kikubwa linamkera mume atakaporudi kutoka kwenye mihangaiko yake.

Hivi unafikiri kwa misingi hiyo mumeo ataacha kutoka nje ya ndoa kweli? Kama unakuwa mchafu wakati wote, humfurahishi, huvutii kama zamani unadhani atafanya nini kama siyo kukusaliti?

Lazima utambue majukumu yako katika ndoa yako. Majukumu yako hayaishii kumfulia, kumpasia na kufanya usafi nyumbani pekee! Majukumu yako ni pamoja na kuhakikisha mumeo anafurahia penzi lako pamoja na kumsaidia katika matatizo mengine ya kikazi na kiakili. Anza kubadilika sasa kabla
KUACHA KUMJALI MWENZAKE
Wakati fulani, baadhi ya wanawake wakishapata mtoto/watoto humsahau mwanaume wake na kuhamishia mapenzi yake kwa mtoto/watoto. Kwamba wanashidwa kugawanya mapenzi vyema kati ya mumewe na mwanawe.

Hili limekuwa tatizo kubwa sana kwa sababu baadhi ya wanawake wakishapata watoto huwasahau kabisa waume zao na kutumia muda mwingi zaidi kuwa na watoto. Wanawake wa aina hii wapo tayari kulala usiku mzima akiwa amemgeukia mwanaye na kumpa mgongo mumewe hadi asubuhi.

Kwa kufanya hivyo wanashidwa kufahamu kuwa mume ataona kuwa hawajali, hivyo kuchochea hamu ya kutafuta hifadhi nyingine nje ya ndoa. Habari mbaya kwao ni kwamba, wanawake wa nje huwa wataalamu na wajanja sana katika suala zima la mapenzi, hivyo kumfanya mwanaume kuwa mpofu dhidi ya mkewe kutokana na kuzama katika mapenzi mazito ya kiruka njia!

Rafiki zangu, mnapaswa kutambua kitu kimoja, japokuwa una mtoto tena anayehitaji mapenzi na huduma zako lakini tambua kuwa una mumeo ambaye pia anahitaji mapenzi yako. Hakika kilio hiki hakiwezi kuisha kama wanawake wa aina hii hawatabadilika na kuwajali waume zao.

Tambua kuwa bila mumeo huyo mtoto wako unayemjali na kushinda naye kutwa nzima ukimmbembeleza kadhalika usiku kucha akiwa ubavuni mwako asingekuwepo! Jitahidi kugawanya mapenzi kwa mwanao na mume wako.

Tambua kuwa wanawake wa nje maarufu kwa jina la vimada ni wajanja sana tena wenye mbinu nyingi za kuwanasa waume za watu wasifurukute kwa lolote kwa kuwapa mapenzi motomoto kiasi cha kuweza kusahau nyumba zao.

TABIA YA ASILI?
Baadhi ya wanaume wana hulka mbaya za kupenda kuwa na wanawake tofauti tofauti kwa minajili ya kuangalia ladha tofauti za mapenzi! Wanaume wa aina hii wapo, hata wakipewa mapenzi ya aina gani hulka hii mbaya waliyonayo huwasukuma kuwa na wanawake wengine wa nje.

Wanaume hawa hupenda kuwa na wanawake tofauti kutokana na tamaa zao za kimwili. Mwanaume wa aina hii ni rahisi sana kumtambua unapokuwa katika uhusiano naye kabla ya kuingia katika ndoa.

Mara nyingi hata unapotoka naye katika matembezi ya jioni au kwenye kumbi za burudani, huweza kusifia mwanamke mwingine aliyepita karibu yenu. Mwanaume wa aina hii hashindwi kukueleza anavyovutiwa kimapenzi na mwanamuziki, mnenguaji au mwigizaji fulani mnapokuwa pamoja katika matamasha yao au mnapoangalia runinga yenu nyumbani.

Tabia za mwanaume wa aina hii huonekana mapema na hivyo ukiona alama hizi ni vyema ukaepukana naye mapema kabla ya kuingia katika ndoa ambayo kwa hakika itakuwa chungu kwako! Wanaume hawa hata ukiwapa mapenzi kiasi gani bado hutoka nje kutokana na hulka yake hiyo mbaya.

ZINGATIO LA MWISHO
Usiruhusu usaliti katika penzi lako, usaliti siyo mzuri hata kidogo katika maisha ya kimapenzi. Unatakiwa kuhakikisha unatumia kila njia kuhakikisha kwamba kunakuwa hakuna usaliti katika penzi lako.

Kwa vipengele hivyo hapo juu, ninaamini kuna mengi mapya uliyojifunza, unachotakiwa kufanya ni kufanya mabadiliko ya dhati katika ndoa yako. Mahali ambapo unahisi ulikuwa unakosea, anza sasa kufanya mabadiliko na uwe mpya katika penzi lako.


Uwezo wa kuruhusu au kukomesha usaliti katika uhusiano wako upo mikononi mwako. Bila shaka umenielewa na utafanya kitu fulani cha tofauti katika maisha yako. Rafiki zangu, mapenzi ni sanaa, kila siku unapaswa kuongeza ujuzi.

Mwisho wake ni kwamba, utakuwa bora kila siku na suala la maumivu kwako litabaki kuwa historia. Niseme nini zaidi ya kukushukuru kwa kutumia muda wako kunisoma? Ahsanteni sana.
hujampoteza mumeo.

No comments:

BREAKING NEWS; MATOKEO YA KIDATO CHA SITA 2018 HAPA

 BFYA LINK HAPA CHINI KUYAPATA>>>>> http://41.59.85.98/results/2018/acsee/acseex.htm

Logo

Logo Design by FlamingText.com