Thursday, November 26, 2015

Kesi ya Pingamizi la Kuuaga Mwili wa Alphonce Mawazo Yaunguruma Mwanza

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza leo imesikiliza kesi ya iliyofunguliwa na familia ya aliyekuwa mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Geita marehemu Alphonce Mawazo. Kesi hiyo ilifunguliwa na baba mdogo wa marehemu, mchungaji Charles Lugiko, huku mlalamikiwa namba moja ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza.
Mawakili wa upande wa jamhuri wamesema mahakamani hapo kuwa kimsingi hawapingani na hoja ya mwili wa marehemu Mawazo kuagwa jijini Mwanza. Hata hivyo, upande huo umeendelea kuonesha mashaka waliyo nayo juu ya kuagwa huko.
Akiwasilisha utetezi wa upande wa mlalamikiwa wa kwanza, wakili wa serikali Emilly Kiria amesema kuwa wanachopinga ni namna na mazingira ya uagaji wa mwili wa marehemu huyo. Wakili mwwingine wa upande wa jamhuri, Seth Mkemwa, alisema kuwa mauaji ya kiongozi huyo yalikuwa ya kikatili, hali ambayo inaweza kuibua hisia kali kwa waombolezaji wakati wa kuagwa kwake.
Makamu Mwenyekiti wa Chadema Taifa Salum Mwalimu akiongea na waandishi wa habari kuhusu kesi ya kuzuiwa kuuaga mwili wa marehemu Mawazo
Mawakili wa upande wa mlalamikaji, James Ole Milya, John Malya na Paul Kipeja waliwasilisha mahakamani hapo maombi ya msingi matatu, wakiiomba mahakama hiyo kutengua amri ya kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza ya kuzuia kuagwa kwa marehemu Mawazo jijini mwanza. Amri hiyo ya mkuu huyo wa polisi ilitaja sababu za zuio hilo kuwa ni kuchukua tahadhari dhidi ya mlipuko wa mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu na kuwepo kwa taarifa za kiintelijensia kuwa kuna tishio la hali ya usalama jijini humo.
Ombi jingine lililowasilishwa na mawakili hao wa mlalamikaji ni kuiomba mahakama itoe agizo kuwa amri hiyo ya kamanda wa polisi wa mkoa wa Mwanza ni batili kisheria, kwani tangazo linalohusiha mlipuko wa magonjwa kama kipindupindu lilipaswa kutolewa na afisa anayetajwa kisheria na linapaswa kutolewa katika gazeti la serikali au katika gazeti lisilo la serikali lenye mzunguko mkubwa katika jamii, na si kamanda wa polisi.
Ombi la tatu lililowasilishwa na mawakili hao ni kuiomba mahakama hiyo itoe agizo la kumkataka kamanda wa polisi wa mkoa wa Mwanza asijihusishe au asiingilie shughuli za msiba na kuagwa kwa mwili wa marehemu Mawazo.
Kesi hiyo inayosikilizwa na Jaji Lameck Mlacha imeahirishwa hadi kesho saa saba mchana ambapo mahakama itakaa kwa ajili ya uamuzi wa kesi hiyo ya msingi.
Mtoto wa marehemu Mawazo ambaye siku chache zilizopita alifanya mtihani wa darasa la nne huku mwili wa baba yake ukiwa kwenye jokofu la kuhifadhia maiti

Wakati hayo yakiendelea, mtoto wa kwanza wa marehemu yupo katika mitihani ya taifa ya darasa la nne iliyoanza jana tarehe 25 Novemba na kutarajiwa kumalizika leo. Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA), watahiniwa wa darasa hilo jana walifanya mitihani ya masomo ya Maarifa ya Jamii, Hisabati, na Lugha ya Kiingereza. Ratiba hiyo inaonesha kuwa leo watahiniwa hao watafanya mitihani ya Sayansi, Kiswahili, Stadi za Kazi, Haiba na Michezo, na Tehama.

Mtoto huyo anafanya mitihani hiyo akiwa katika wakati mgumu huku akifahamu unyama uliotumika kumkata kata baba yake hadi kufa, na pia akifahamu kuwa mpaka sasa mwili wa mzazi wake huyo umehifadhiwa katika jokofu la maiti katika chumba cha kuhifadhia maiti, huku pia kukiwa na mvutano wa kisheria juu ya shughuli ya kuuaga mwili wake.

No comments:

BREAKING NEWS; MATOKEO YA KIDATO CHA SITA 2018 HAPA

 BFYA LINK HAPA CHINI KUYAPATA>>>>> http://41.59.85.98/results/2018/acsee/acseex.htm

Logo

Logo Design by FlamingText.com