Friday, June 19, 2015

JE WAJUA WANAWAKE WANAVUTIWA NA NINI ZAIDI KWA WANAUME? ZAMA HAPA KUJUA ZAIDI

Kama mwanaume lazima upate wakati 
wa kujua unatakiwa kufanya nini kwa 
ajili ya kulifanya penzi lako lizidi 
kuchanua. 
USAFI BINAFSI 
Asilimia kubwa ya wanawake 
wanapenda sana usafi. Ni aghalabu sana 
kukutana na mwanamke asiyejipenda. 
Ndiyo maana wanaitwa mapambo ya 
nyumba au la nyumba! Ni kwa sababu 
ya hulka yao ya kupenda sana usafi. 
Mwanamke anavutiwa sana na 
mwanaume mtanashati. Usafi wako 
unamfanya ajiamini kuwa na wewe. 
Hata nyumbani kwako, lazima uishi 
katika nyumba safi. Hata anapokuja 
kukutembelea, anakuta mazingira 
masafi kuanzia sebuleni hadi chumbani. 
Anapokukuta katika hali ya usafi, 
inakuwa rahisi zaidi yeye kuanzia hapo 
alipokukuta na kuendelea mbele. 
KUJIAMINI 
Mwnamke anajisikia salama zaidi akiwa 
na mwanaume ambaye anajiamini – 
mwenye uwezo wa kutetea hoja zake na 
kujieleza sawia. Siyo anayebabaika. Suala 
la msimamo binafsi, kwa mwanamke ni 
kubwa kuliko hata kumnunulia 
manukato mapya! 
Mathalani unakuwa naye katika mtoko, 
angependa kukuona ukiwa katika hali 
halisi ya maisha yako, usiyeyumbishwa 
na mwenye kutoa maamuzi 
yasiyoyumba. 
Wakati mwingine, mwanamke anaweza 
kukupima hata katika jambo ambalo 
amekosea yeye, ataangalia unavyotoa 
maamuzi yako, lakini pia atafuatilia 
kuona kama utakuwa mwepesi wa 
kuyabadilisha. 
Anataka kuona msimamo wako muda 
wote. Mwenye kujiamini na mawazo 
yasiyo na matege wala makengeza! 
KUJITETEA 
Kipengele hiki hakina tofauti kubwa 
sana na kilichopita, lakini hapa ni 
kwenye upande wa kujitetea zaidi. 
Wakati unapodai haki yako mbele ya 
mwanamke wako, suala la kujitetea 
linapewa nafasi kubwa sana. 
Wanawake hawapendi kuwa na 
wanaume ambao wapo tayari kuonewa. 
Wanataka wenye uwezo wa kusimama 
kidete kuona haki zao hazichukuliwi 
kirahisi. 
Hili si suala la kutetea tu haki yako pekee 
kama mwanaume, bali inapobidi 
kusimamia haki ya mwanamke wako. 
Nisieleweke vibaya katika hili, lakini 
mwanaume imara ni yule ambaye ana 
nguvu – anafanya mazoezi na ambaye 
yupo tayari kwa lolote! 
Inapowezekana, uwe na uwezo wa 
'kuzichapa' ikiwa mtakutana na vibaka 
au watu wabaya wenye lengo wa 
kukudhuru/kuwadhuru au kumdhuru 
mpenzi wako. 
Mwanaume aliye 'fiti' ni chaguo la 
wanawake wengi. Si mnyonge. Mpole 
kupitiliza na aliye tayari kuonewa! Huyu 
hana nafasi. 
KUJALI 
Wanawake wanapenda sana wanaume 
wanaojali. Wanawaona wao ni kila kitu 
na wanaotoa kipaumbele kwao. Kama 
huna tabia hiyo, ujue upo katika nafasi 
kubwa ya kumkwaza mpenzi wako. Mjali 
mpenzi wako kwa kila hali. 
Kumjulia hali kila wakati na kutaka kujua 
maendeleo yake, kutakupa nafasi kubwa 
sana ya kuendelea kudumu katika 
uhusiano hai. 
UKARIBU 
Kati ya vitu vinavyowapa mshawasha 
mkubwa wanawake ni pamoja na 
kusogezwa karibu. Hapa ni kuwa naye 
katika mambo mengi unayoyafanya kila 
siku. 
Ni vizuri kuwasiliana naye mchana, 
ukitaka kujua aina ya chakula alichokula 
siku hiyo au ikiwezekana mchagulie. Ni 
mambo madogo sana lakini 
yanayoongeza nakshi katika mapenzi. 
Yapo mengi sana ambayo kwa 
kuyafanya utakuwa umemsogeza 
mpenzi wako karibu yako. Hebu tumia 
ubunifu wako ili uweze kuteka hisia za 
mwenzi wako kisawasawa! 
KUMSIFIA 
Wanaume wengi hupuuzia hili, huona 
kama ni jambo lisilo na maana sana 
kwao na wenzi wao. Hali ni tofauti sana 
kwa wanawake ambao hupenda 
kuwasifia wanaume zao. Nitakupa 
mifano miwili ya namna wanandoa wa 
jinsia mbili tofauti 
wanavyotambulishana kwa jamaa zao. 
MWANAUME: "Peter kutana na mke 
wangu, anaitwa mama Diana. Nipo naye 
mwaka wa tatu sasa, tuna watoto 
wawili, huyo Diana na mwingine 
anaitwa Cris. Mama Diana, huyu ni Peter 
nilisoma naye A – Level, Tosamaganga 
Sekondari." 
MWANAMKE: "Suzan, huyu ndiye mume 
wangu mpenzi...anaitwa Elifaraja lakini 
mimi napenda zaidi kumuita Elly. 
Kiukweli nampenda sana mume wangu 
jamani, tuna mtoto wetu mmoja, 
anaitwa Agness. (Akimgeukia mumewe) 
Baby, huyu hapa ni rafiki yangu Suzan. 
Yaani tumekua naye mtaa mmoja huko 
Arusha." 
ANGALIA TOFAUTI 
Bila shaka kwa namna wawili hao 
walivyotambulishana unaweza kuona 
tofauti kubwa. Mwanaume 
amemtambulisha mkewe kawaida 
kabisa, hajaonesha manjonjo au namna 
anavyompenda na kumthamini 
mwenzake, lakini mwanamke amefanya 
hivyo. 
Sikia nikuambie, KUMSIFIA mwanamke, 
kuna nafasi kubwa sana kwake. 
Chunguza kwa makini, hata 
kunapokuwa na mgongano katika 
familia, halafu wakatokea wageni, baada 
ya utambulisho na mazungumzo ya 
hapa na pale, wageni wakiondoka 
kunakuwa na uwezekano mkubwa zaidi 
wa kumaliza mpasuko katika familia. 
Jenga utamaduni wa kumsifia mpenzi 
wako, unamuweka katika kilele cha 
upendo. Anajiona kamili, peke yake na 
mwenye nguvu kwako. Anajiamini na 
unamfanya azidi kukupenda kwa kuwa 
anaamini yupo na mwanaume ambaye 
anajivunia kuwa naye. 
MALENGO 
Wanaume wengi wana ulemavu mmoja; 
hawapendi kuwashirikisha wanawake 
katika mambo yao. Wanapenda kufanya 
mambo yao kwa siri na wakati 
mwingine ikilazimika kumwambia 
mkewe basi kwa mshtukizo baada ya 
kukamilisha jambo husika. 
Hii si sahihi. Dunia ya leo imebadilika 
rafiki zangu. Inawezekana wazee wa 
zamani walikuwa sahihi, maana ilikuwa 
ni suala la kununua ng'ombe na 
kuwaweka katika zizi kwenye kijiji cha 
jirani, halafu wanapewa malisho mazuri, 
baada ya miaka miwili wanazaliana, 
hapo ndipo anamweleza mkewe. 
Siku hizi dunia imebadilika, kuna mambo 
mengi. Kuna suala la hasara katika 
biashara, utapeli n.k. Mkeo ndiye rafiki 
yako mkubwa kuliko wote, ndiye ndugu 
yako wa karibu zaidi kuliko yeyote. Yes! 
Mkeo ndiye ndugu yako maana 
umetengeneza naye familia. 
Mmeshirikiana kuzaa watoto na kujenga 
maisha pamoja. 
Yeye anapaswa kujua mambo yako, 
ndiye mtetezi wako nambari wani. 
Mweleze juu ya malengo yako, wakati 
mwingine anaweza kukusaidia sehemu 
ambayo hukutarajia. 
Hata hivyo, kumshirikisha katika 
malengo yako, kunampa nguvu na 
nafasi ya kujiona mama katika familia 
yenu. Msaidizi kamili wa nyumba yenu. 
KIPAUMBELE 
Kuna wakati wanawake huwa na 
mambo yao binafsi. Kazini au kifamilia. 
Inawezekana akatatizika katika eneo 
fulani ambalo kwa namna moja ama 
nyingine atahitaji usaidizi wako. Ikitokea 
mkeo akawa katika hali hiyo, msikilize. 
Mathalani ana tatizo la kifamilia, 
amekuambia mmoja wa wazazi wake 
anaumwa, msaidie. Si lazima kifedha, 
lakini kuonesha kujali kwako tu, 
kutampa matumani kwamba anaishi na 
mtu sahihi. Acha kupuuza mambo yake; 
hata yale madogo, kama ya 'mtoto wa 
dada amerudishwa ada shuleni'. 
Msikilize, mshauri panapofaa kufanya 
hivyo na ukiweza msaidie hata kifedha. 
Katika upande wa pili ni hivyo hivyo. 
Labda una tatizo binafsi, kazini kwako 
au kifamilia, mshirikishe. 
Unaweza kushangaa jambo ambalo 
uliamini unaweza kulimaliza peke yako, 
kwa kumshirikisha likawa jepesi zaidi na 
mambo yakaendelea vyema. Kipaumbele 
kwa namna yoyote ile, kunaongeza 
mapenzi zaidi kwa mwanamke. 
TENDO LA NDOA 
Hiki ni kipengele nyeti, kinachohitaji 
lugha nzuri ya kirafiki kukifafanua. 
Hakuna siri, tendo la ndoa ni moja ya 
kiwakilishi cha ndoa. Maana hata 
maandiko yanasema: "Mwanamke 
ataacha wazazi wake na kwenda kwa 
mumewe, nao watakuwa mwili mmoja." 
Kimsingi tendo la ndoa lina nafasi yake. 
Ni muhimu likaheshimiwa na 
kutengewa muda maalum wa kufurahia. 
Si papara. Kwa bahati mbaya wanaume 
huwa si wafuatiliaji sana wa kujua 
namna ya kuwafurahisha zaidi wenzao. 
Wenyewe wanajiwazia wenyewe. 
Wanafikiria namna ya kuwakomoa 
wenzao. 
Si sahihi. 
Tendo la ndoa halina maana ya 
kukomoana. Jenga mazoea ya kufanya 
maandalizi kamili kabla ya tendo. Sikiliza 
hisia za mwenzako. Ukiweza kumjulia 
mke wako katika eneo hili, ni wazi 
kwamba utazidisha upendo wake 
kwako, lakini pia atakuwa katika kuta za 
uaminifu. Akatafute nini nje wakati 
wewe ndiye mganga wake unayeweza 
kumtibu barabara? 
Kuna kitu nimesahau kweli? Kama kipo 
nitafute pembeni, kwa hapa haya 
yatoshe kukufanya uelewe nilichotaka 
kukuelekeza. Nikuache na neno moja; 
uamuzi wa kuijenga ndoa yako upo 
mikononi mwako. Ukitaka iwe 
shaghalabaghala, pia ni wewe tu!

No comments:

BREAKING NEWS; MATOKEO YA KIDATO CHA SITA 2018 HAPA

 BFYA LINK HAPA CHINI KUYAPATA>>>>> http://41.59.85.98/results/2018/acsee/acseex.htm

Logo

Logo Design by FlamingText.com