Wednesday, May 13, 2015

MKASA WA KUSIKITISHA HUKO KAHAMA..BIBI KIZEE ATWAJWA KUHUSIKA KULETA MVUA HIYO BAADA YA KUTUHUMIWA KUPOTEZA MVUA





MENGI yamesemwa na yanaendelea kusemwa kufuatia mvua kubwa iliyonyesha wilayani Kahama, Shinyanga na kuua watu 45 huku wengine 92 wakijeruhiwa, achilia mbali waliopoteza makazi yao.
Habari za hivi karibuni zinadai kuwa, mvua hiyo licha ya kutabiriwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) lakini wakazi wa maeneo hayo wanaamini ina mkono wa bibi kizee ‘kikongwe’ mmoja ambaye hakutajwa jina.
Muonekano wa nyumba baada ya kuanguka kutokana na mvua kubwa iliyonyesha wilayani Kahama, Shinyanga na kuua watu 45 huku wengine 92 wakijeruhiwa.
WALICHOSEMA WAKAZI
Masanja, ni mkazi wa Kahama ambaye ameliambia Uwazi mwishoni mwa wiki iliyopita kwamba, bibi kizee huyo hivi karibuni aliingia kwenye mgogoro na wakazi wa eneo hilo wakimtuhumu kwamba, amekuwa akizuia mvua na kulifanya eneo hilo kuwa kame kwa muda mrefu.
“Sitaki kukitaja jina kijiji alichotoka lakini huyu bibi, baada ya mzozo mkubwa aliamua kuondoka na kuahidi kuwa, kama tunataka mvua basi atatuletea kiasi kikubwa mpaka kushindwa kuizuia,” alisema Masanja.
HAIJAWAHI KUTOKEA

Masanja aliendelea kusema kuwa, kwa kiasi kikubwa cha mvua iliyonyesha wilayani humo, haijawahi kutokea tangu kuzaliwa kwake hadi umri alionao kwa sasa, miaka 43.

BIBI KIZEE HAJULIKANI ALIPO
Kwa mujibu wa watu wa eneo lililokumbwa na mafuriko hayo, mpaka sasa kikongwe huyo hajulikani alipo huku baadhi ya vijana waliopoteza ndugu mbalimbali wakiahidi kumfanyia kitu mbaya punde watakapomweka machoni.
Mwili wa marehemu (katikati) aliyepoteza maisha kutokana na mvua hiyo akiwa amebebwa na wananchi eneo la tukio.
ALIYEPOTEZA MKE, WATOTO NA MAMA ASIMULIA
Naye Emmanuel Lyankanda (37) , mkazi wa Kijiji cha Mwakata wilayani hapa ambaye ameachwa katika majonzi makubwa baada ya kuwapoteza watoto wake watano, mama yake mzazi  na mkewe amesimulia mapya kuhusu mvua hiyo.
Akizungumza na Uwazi kijijini hapo mwishoni mwa wiki iliyopita, Lyankanda alisema:
“Sikumbuki hasa ilikuwa saa ngapi lakini nadhani ni majira ya saa nne kasoro usiku, ghafla ulianza upepo mkali uliomshtua kila mtu. Hali ikawa tete, lakini kabla haijajulikana ni nini, mara mvua kubwa ilianza kunyesha tena ikiambatana na na mawe  makubwa ya barafu.”

Mwananchi akiwa amebeba mwili wa marehemu.
ALIKUWA KWA RAFIKI YAKE
Mwanaume huyo aliendelea kusema kuwa, wakati mvua hiyo kubwa inaanza kuporomoka yeye alikuwa nyumbani kwa rafiki yake alikokwenda kumsalimia.

“Nilipoona mvua ni kubwa kupita kawaida, nilitaka kukimbilia nyumbani lakini nilishidwa kwani nilipotoka nje tu nilipigwa na jiwe la barafu kichwani na kunilazimu kurudi tena ndani kwa rafiki yangu.
“Ilitulazimu tujifungie ndani lakini rafiki yangu alifungua mlango ili akachukue baiskeli yake nje lakini hakurudi tena baada ya kukumbana na jiwe la barafu ambalo lilimpiga kichwani na kuanguka. Alipotajihidi kuinuka alipondwa na mawe mengine na kufa papohapo.”
Mwananchi akiwa amebeba jiwe la barafu.
Lyankanda aliendelea kusema kuwa, kutokana na mvua kubwa kuzidi kunyesha huku upepo mkali ukivuma na radi, alisikia vilio vya watu wazima na watoto kutoka pande zote za kijiji, anasema: “Hakika niliogopa sana kwani tangu nizaliwe sijawahi kuona hali kama hii.
“Nataka kusema kutoka moyoni kwamba, mimi nilijua siku ile ndiyo mwisho wa dunia, nilitamani sana nikimbilie nyumbani kuiona familia yangu lakini nilishindwa. Niliogopa sana, nikainama na kusali sala ya mwisho maana mwisho wa dunia umefika.”
Akasema: “Nikiwa katika hali ya shaka, ghafla paa la nyumba ya rafiki yangu ambaye mwili wake ulikuwa umelala nje kwenye mvua, liliniangukia, nilisikia maumivu makali na nikaona giza kisha sikujua tena kilichoendelea, nilipoteza fahamu,” alisema Emmanuel huku akitokwa machozi.
“Nilipozinduka nilisikia baridi kali na kichwa kilikuwa kizito na kikiuma sana. Nilisikia sauti za watu wakilia. Nilipojaribu kuinuka nikashindwa kwani nilikuwa nimegandamizwa na paa la nyumba, lakini nikajitahidi nikafanikiwa kuchoropoka hapo.”

KWAKE AKUTA MAITI
“Hali ilikuwa mbaya, nililowa chapachapa, nilikimbia kwa shida huku nikiyumba  hadi nyumbani lakini nilichokikuta sikuyaamini macho yangu. Nyumba yangu ilikuwa imeanguka.
“Nilijitahidi kuinua paa la nyumba, da! Niliikuta familia yangu yote imelaliana, wote ni marehemu. Nilipiga kelele lakini sikupata msaada kutoka kwa mtu yeyote, kumbe lilikuwa janga la kijiji kizima.
Lyankanda aliwataja marehemu wapendwa wake kuwa ni mkewe, Christina Machanga, wanawe Monica Homo, Hoja Homo, Limi Homo, mama yake mzazi, Pendo Lyakanda na mdogo wake, Miligo Lyankanda.

Mbuzi wakiwa wakiwa wamefariki kutona na mvua hiyo.
ANATAKA KUHAMA
Alisema kuwa anafikiria kuhama kijijini hapo kila anapoiona nyumba yake na kila anapokwenda makaburini ilikozikwa familia yake.
Hivi karibuni, TMA walisema kuwa, mvua kubwa iliyonyesha Kahama haikuwa ya kawaida licha ya utabiri wao kuonesha kuwepo kwa mvua hiyo.

No comments:

BREAKING NEWS; MATOKEO YA KIDATO CHA SITA 2018 HAPA

 BFYA LINK HAPA CHINI KUYAPATA>>>>> http://41.59.85.98/results/2018/acsee/acseex.htm

Logo

Logo Design by FlamingText.com